MKURUGENZI MAGESA ATOA SIKU 30 KUKAMILISHA MIRADI, WASIMAMIZI WATIA SAINI MKATABA WA MAKUBALIANO YA UTENDAJI KAZI (PERFORMANCE AGREEMENT CONTRACT).
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Ndg. Philemon Mwita Magesa, amefanya kikao kazi na Wasimamizi wa Miradi wa Halmashauri hiyo, ambapo wametia saini Mkataba wa Makubaliano ya Utendaji Kazi (Performance Agreement Contract) kwa lengo la kuhakikisha miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati, kwa ubora na kwa kuzingatia thamani ya fedha ya Serikali.
Kikao hicho kimewakutanisha Wakuu wa Idara na Vitengo vyote, Waganga Wafawidhi, Watendaji wa Kata, Wakuu wa Shule, Maafisa Elimu Kata pamoja na Walimu Wakuu kutoka kata zote 21 zilizopo ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Magesa ametoa siku 30 pekee kwa Wasimamizi wa Miradi kukamilisha miradi yote inayotekelezwa katika kata zao, akisisitiza kuwa hakutakuwa na uvumilivu kwa uzembe, uzorotaji wa kasi wala kukiuka viwango vilivyopangwa.
Aidha, Magesa amewataka Wasimamizi wa Miradi kuwabainisha wazi wazabuni na wakandarasi/fundi wote wanaosababisha usumbufu katika utekelezaji wa miradi, ikiwemo kuchelewesha usambazaji wa malighafi na kutotekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mikataba, ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao bila kusita.

Mkataba huo wa Makubaliano ya Utendaji Kazi umetiwa saini tarehe 31 Januari, 2026, na umeanza rasmi kutekelezwa leo tarehe 1 Januari, 2026, ambapo baada ya muda uliopangwa kila msimamizi atawajibika kukabidhi mradi wake ukiwa umekamilika kwa asilimia 100.
Mkataba huo umetiwa saini na Wasimamizi wa Miradi na kushuhudiwa rasmi mbele ya Mwanasheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Wakili Walter Kaijage.
Hatua hiyo inalenga kuongeza uwajibikaji, ufanisi na kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi wa Wilaya ya Namtumbo.
Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo
Anuani: 2 Barabara ya Boma, S.L.P 55, 57382 NAMTUMBO
Simu ya Mezani: 0252675008
Simu ya Mkononi: 0767519181
Barua Pepe: ded@namtumbodc.go.tz
Hakimiliki©2021Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo. Haki zote Zimehifadhiwa.