Magesa ameyasema hayo katika kikao na Wasimamizi wa Miradi kilichofanyika katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Nasuli, ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Ndg. Philemon Mwita Magesa, ametoa maagizo kwa wasimamizi wa miradi yote ya maendeleo kuhakikisha utekelezaji unafanyika kwa mfumo wa usiku na mchana, kwa kuzingatia ubora, viwango na miongozo iliyopangwa na Serikali.
Akizungumza katika kikao hicho, Ndg. Magesa alisisitiza kuwa Serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi ya maendeleo kwa lengo la kuboresha huduma kwa wananchi, hivyo ni wajibu wa watendaji na wasimamizi wote kusimamia ipasavyo utekelezaji wa miradi hiyo bila uzembe, ucheleweshaji wala kukiuka taratibu.
“Kila mradi lazima utekelezwe kwa kasi, lakini kasi hiyo iende sambamba na ubora. Hakikisheni mnasimamia viwango vyote vya kitaalamu kama ilivyoelekezwa, kwani miradi hii ni kwa manufaa ya wananchi,” alisema Ndg. Magesa.
Katika kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji alionekana ameketi pamoja na waganga wafawidhi, watendaji wa kata, wakuu wa shule, waratibu wa elimu kata pamoja na walimu wakuu, ambapo kwa pamoja walijadili changamoto na mikakati ya kuimarisha usimamizi wa miradi, hususan katika sekta za elimu na afya.
Aidha, Ndg. Magesa aliwataka viongozi hao kushirikiana kwa karibu, kutoa taarifa za mara kwa mara za maendeleo ya miradi, na kuchukua hatua stahiki dhidi ya uzembe wowote unaoweza kujitokeza, ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaokidhi matarajio ya Serikali na wananchi wa Wilaya ya Namtumbo.